AZONTO AWASILI DAR, KUFANYA MAKAMUZI YA NGUVU KESHO

Mwanaumzi Fuse ODG (wa pili kulia) akiserebuka ngoma yake ya Azonto pamoja na waandishi wa habari.

Fuse ODG akizungumza na waandishi wa habari, (hawapo pichani) na kulia ni Afisa Biashara Mkuu wa Zantel, Sajid Khan na kushoto ni Mkurugenzi wa Radio ya Times FM, Rehure Nyaulawa.
Fuse ODG akipozi na wanahabari.
Fuse ODG akitoka katika Hoteli ya Kilimanjaro baada ya mkutano wake na waandishi.
Mwanamuziki mahiri kutoka nchini Ghana, Fuse ODG, aliyewasili leo jijini Dar es Salaam, ameahidi kufanya makamuzi ya kufa mtu kesho.
Akizungumza kwenye mkutano na Waandishi wa habari uliofanyika katika Hoteli ya Kilimanjaro, Posta alasiri leo, Fuse alisema amefurahi kufika Tanzania na kuwaahidi wapenzi wa burudani hususan wa nyimbo zake ukiwano wa Azonto kuwa watapata kile kitu roho inapenda.
Afisa Biashara Mkuu wa Zantel, Sajid Khan aliyeongozana na mwanamuziki huyo kwenye mkutano huo wa Waandishi wa Habari alisema Zantel imemleta mwanamuziki huyo ili kuwapa ari wasanii wa ndani wenye lengo la kufikisha kazi zao hatua ya kimataifa.
“Zantel imekuwa mstari wa mbele katika kuwawezesha wasanii wa ndani, hasa vijana, na kwa kumleta Fuse ODG, ambaye ni mmoja wa wasanii wachache kutoka Afrika waliofanikiwa kufikisha muziki wao soko la kimataifa, tunaamini vijana watajifunza mengi,” alisema Khan.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Radio Times FM, Rehure Nyaulawa alisema wamemleta msanii huyo ili kuhakikisha Watanzania wanapata burudani wanayoipenda ya Azonto hapa nchini.
“Azonto imejipatia umaarufu mkubwa karibu dunia nzima, lakini pia kwa upande wa radio yetu wimbo huu umepata maombi mengi kuliko wimbo wowote wa kimataifa kiasi cha kuona tuwaletee Watanzania burudani wanayoipenda,” alisema Nyaulawa.
Shoo ya mwanamuziki huyo itafanyika kesho katika Viwanja vya Chuo cha Ustawi wa Jamii Kijitonyama na burudani itaanza saa mbili usiku hadi majogoo.
Kiingilio katika shoo hiyo kitakuwa shilingi 10,000 kwa kununua tiketi kabla na shilingi 15,000 kwa kununua mlangoni.

No comments:

Post a Comment