HONGERA YANGA KWA KUTWAA NGAO YA JAMII KWA KUWAPIGA AZAM FC RISASI 1-0… LAKINI JICHO LA TATU LIMEBAINI UBORA WA LUHENDE NA UGONJWA WA TAIFA WA UBUTU WA SAFU YA USHAMBULIAJI !!
Wakati
 mashabiki wakifurika kwa wingi kwenda kuutazama mchezo wa ngao ya jamii
 hapo jana baina ya mabingwa wa ligi kuu Tanzania bara, klabu ya Yanga 
dhidi ya Makamu bingwa, Wana Lambalamba Azam fc katika uwanja wa Taifa 
jijini Dar es salaam, binafsi sikwenda kushangilia timu yoyote bali 
nilienda kushuhudia mambo makubwa mawili.
Mechi
 ya jana kwa upande wangu ilikuwa burudani kubwa sana kwani nilishuhudia
 soka safi la ushindani, kwani timu zote “zimefundwa” kiukweli.
Maarifa
 ya makocha wawili wa kizungu, Ernie Brandts kwa Yanga na Sterwart John 
Hall wa Azam, yanaonekana kuwakolea vijana wa Kitanzania na nje ya 
Tanzania wanaozichezea timu hizo mbili.
Ukihusianisha
 majina ya “Yanga na Azam fc” hayana ushindani, na hii inatokana na 
Yanga kuwa klabu kongwe zaidi hapa Tanzania na imejiimarisha kwa kuwa na
 mashabiki lukuki zaidi ya Azam ambao ndio kwanza wameanza safari yao, 
lakini kwa kuangalia aina ya mpira unaochezwa na timu hii yenye makazi 
yake Chamazi, najiridhisha kuwa ni timu bora iliyojipanga na itafika 
mbali.
Inafahamika
 kuwa mechi ya jana hiyo ilimazika kwa Yanga kushinda kwa bao 1-0, bao 
likifungwa na Salum Abdul Telela katika dakika ya pili tu, watoto wa 
mjini huita “Dakika za Asubuhi”, kwangu mimi matokea hayana maana sana, 
lakini  nilijivuta kwenda uwanja wa Taifa kwa  mambo mawili kama 
nilivyosema hapo juu.
Nahodha
 wa Yanga, Nadir Haroub “Canavaro” akipokea ngao ya jamii kutoka kwa 
mgeni Rasmi, mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Mhe. Said Meck Sadick
Kwanza,
 nilienda kumuangalia bwana mdogo aliyeshutumiwa na mashabiki wengi wa 
soka nchini kwa kusababisha penati na kuwa uchochoro wakati  Taifa Stars
 ilipofungwa na Uganda mabao 3-1 jijini Kampala kuwania kucheza fainali 
za CHAN,  huyu si mwingine bali ni kinda David Luhende.
Watu 
walizungumza sana juu ya uwezo wake,wengine walisema kocha Kim alikosea 
kumpanga mechi yake ya kwanza Taifa Stars  dhidi ya Uganda, mechi kubwa 
ya mashindano na alikuwa uchochoro, lakini wakasahau kuwa hata “Mbuyu 
ulianza kama mchicha”. Binafsi nilijiridhisha kuwa atakuwa bora zaidi 
kwa uwezo alioonesha kwa siku ya kwanza, licha ya kuwa na mapungufu.
Naupenda
 sana msemo wa kocha wa klabu ya Mbeya City ya jijini Mbeya, Juma 
Mwambusi, huwa anasema “Mchezaji yeyote mwenye uzoefu alianza kutokuwa 
na uzoefu, akapewa nafasi akacheza na baadaye kupata uzoefu, hivyo 
lazima wachezaji wote wapate nafasi ya kucheza ndipo wajenge uzoefu, 
usipompa nafasi kijana atatoa wapi uzoefu”?.
Nina 
uhakika hata kocha wa Stars, Kim Poulsen ana falsafa hiyo ya kuwaamini 
wachezaji vijana na kuwapa majukumu mazito kama alivyofanya kwa David 
Luhende ambaye aliitwa kwa mara ya kwanza Taifa stars mwezi uliopita na 
kucheza mechi ngumu ya mashindano dhidi ya Uganda.
Ukitaja
 jina la Luhende, wapenda michezo wengi waliokuwa na malengo ya kwenda 
Afrika kusini kushuhudia fainali za kombe la mataifa ya Afrika kwa 
wachezaji wa Ligi za ndani, CHAN nywele zinawasisimka kutokana na madudu
 aliyofanya nyota huyo kinda baada ya kuitwa kuziba pengo la Shomary 
Kapombe aliyekwenda Ulaya kujaribu bahati yake ya kucheza soka la 
Mataifa.
Luhende
 alikuwa uchochoro vibaya sana kwani alipitisha mipira mingi ya hatari 
na kuunawa mpira katika eneo la hatari na mwamuzi kuwazawadia mkwaju wa 
penati Uganda na kufunga bao la pili kupitia kwa nyota wao Brian Majwega
 na kuwachanganya stars waliolala kwa mabao 3-1.
Jana 
bila kuwa na roho ya kinyongo,  bila kujali unazi wa timu, Luhende 
alipiga mpira mkubwa sana na ilikuwa burudani kubwa wanapokutana na 
Khamis Mcha “Vialli” wa Azam, ufundi mkubwa ulioneshwa na hii inaashiria
 hatari kwa beki wa kushoto wa Yanga, Oscar Samwel Joshua.


No comments:
Post a Comment