Ukiyazingatia Mambo Haya 5 Unaweza Kupata Kazi/Ajira Ndani ya Siku 60

NI NANI hupata kazi bora? Je, ni yule anayestahili zaidi? “La hasha,” anasema Brian, mshauri wa kazi. “Mara nyingi yule anayetafuta kazi akitumia mbinu nzuri ndiye hufanikiwa.” Unaweza kutumia mbinu gani kutafuta kazi? Haya hapa ni madokezo matano.

1. Uwe Mwenye Utaratibu
Ni rahisi kuvunjika moyo ikiwa umepoteza kazi nzuri au hujaajiriwa kwa muda fulani. Katharina, mfanyabiashara ya soko la mtandao aliyeko hapa Dar es Salaam anasema, “Nilipopoteza kazi, nilitumaini kwamba nitapata nyingine. Lakini nilishuka moyo kadiri miezi ilivyopita bila kupata kazi. Mwishowe, hata ilikuwa vigumu kwangu kuzungumza kuhusu jambo hilo na rafiki zangu.” Hakika alikuwa alikuwa amekata tamaa.


Aliwezaje kukabiliana na hisia za kukata tamaa? Kitabu Get a Job in 30 Days or Less kinasema, “Inafaa upange ratiba yako kama ‘siku ya kazi’ ya kawaida ili uanze siku ukijua unapaswa kufanya nini.” Waandishi wa kitabu hicho wanapendekeza kwamba “uweke miradi ya kila siku na uandike ulichotimiza.” Kwa kuongezea, wanasema kwamba “kila siku unapaswa kuanza kwa kuvalia kana kwamba unaenda kazini.” Kwa nini? “Kuvalia inavyofaa kutafanya uweze kujiamini zaidi hata unapozungumza kwenye simu.”

Unapaswa kuona kazi ya kutafuta kazi kuwa ndiyo kazi yako, haidhuru itakuchukua muda mrefu kadiri gani. Katharina, aliyetajwa hapo awali alifuata utaratibu huo. Anasema hivi: “Nilipata anwani na namba za simu za waajiri kutoka kwenye ofisi ya serikali ya kusaidia watu kupata kazi. Nilijibu matangazo yaliyochapishwa kwenye magazeti. Nilichunguza kitabu cha simu na kuandika orodha ya kampuni ambazo zingeweza kuwa na nafasi za kazi ambazo bado hazikuwa zimetangazwa, kisha nikawasiliana nazo. Pia niliandika habari fupi kuhusu elimu na ujuzi wangu na kuituma kwa kampuni hizo.” Baada ya kutafuta kazi akitumia utaratibu huo, Katharina alipata kazi nzuri.

2. Tafuta Kazi Ambazo Hazijatangazwa
Mvuvi mwenye wavu mkubwa zaidi ndiye mwenye uwezekano mkubwa wa kuvua samaki. Vivyo hivyo, kujua jinsi ya kupanua “wavu” wako kutafanya uwe na uwezekano mkubwa wa kupata kazi. Ikiwa unatafuta kazi kwa kujibu tu matangazo yaliyo kwenye magazeti au kwenye Intaneti, huenda ikawa unapitwa na kazi nyingi. Ukweli ni kwamba kazi nyingi hazitangazwi. Unawezaje kutafuta kazi hizo?

Mbali na kujibu matangazo kama alivyofanya Katharina, unapaswa kutenga wakati kila juma wa kupiga simu kwa kampuni ambazo unafikiri huenda zikawa na kazi unazoweza kufanya. Usingoje hadi kazi hizo zitangazwe. Meneja akikuambia kwamba hakuna kazi, mwulize ikiwa anajua kampuni zilizo na nafasi za kazi na mtu unayepaswa kuzungumza naye. Akipendekeza kampuni fulani, panga kuwasiliana na kampuni hiyo ukitaja jina la mtu aliyekutuma.

Wapo baadhi ya marafiki zangu waliopata kazi kwa njia hiyo. Mmoja wa marafiki hao kwa jina la Tony alinieleza hivi: “Niliwasiliana na kampuni hata ingawa hazikuwa zimetangaza nafasi za kazi. Kampuni moja ilisema kwamba haikuwa na nafasi zozote wakati huo lakini ikaniambia nijaribu tena baada ya miezi mitatu. Nilifanya hivyo na nikapata kazi.”

Rafiki yangu mwinine aitwaye Anna anayeishi Mwanza, alitumia mbinu kama hiyo. Anasema: “Nilipokuwa nikihudhuria masomo ya kutoa huduma ya kwanza, niliona jengo jipya likijengwa upande ule mwingine wa barabara na nikagundua kwamba litakuwa pango  la ofisi. Nilijaribu mara kadhaa kukutana na msimamizi wa msimamizi wa jengo hilo. Mwishowe aliniambia kwamba hakukuwa na nafasi za kazi wakati huo. Hata hivyo, nilirudi mara kwa mara ili kuona kama ninaweza kufanya kazi mahali hapo, hata kama ni ya kujitolea. Hatimaye, niliajiriwa kazi ya muda. Nilifanya kazi zozote nilizopewa kwa bidii. Kwa sababu hiyo, nilipata ujuzi zaidi na kupata kazi ya kudumu kwenye moja ya makampuni yaliyokuwa na ofisi zao mule.”

Pia unaweza kuwauliza marafiki wako, familia, na watu wengine wakusaidie kutafuta kazi ambazo hazijatangazwa. Hivyo ndivyo Jacob, ofisa wa fedha katika shirika moja huko Arusha alivyopata kazi. Anasema: “Wakati kampuni niliyokuwa nikifanyia kazi ilipofilisika, niliwajulisha marafiki na watu wa familia kwamba ninatafuta kazi. Siku moja rafiki yangu mmoja alisikia mazungumzo fulani alipokuwa katika foleni ya kulipia bidhaa zake kwenye super market. Mwanamke mmoja alikuwa akimwuliza mwenzake ikiwa anajua mtu yeyote anayetafuta kazi. Rafiki yangu aliingilia mazungumzo hayo na kumwambia kunihusu. Mipango ilifanywa na nikapata kazi hiyo.”

3. Uwe Mwenye Kubadilika
Ili uongeze nafasi za kupata kazi, lazima uwe mwenye kubadilika.Edwin, ambaye ni Afisa utumishi katika moja ya benki kubwa hapa nchini yeye husisitiza: “Kuna uwezekano mkubwa kwamba hutapata kazi unayotarajia. Unapaswa kujifunza kuridhika na kazi isiyopatana na matarajio yako.”

Kuwa mwenye kubadilika kunamaanisha kutochagua kazi fulani. Mfikirie Ericka, anayeishi Dar es Salaam. Ingawa alisomea kazi ya katibu muhtasi, mwanzoni hakuweza kupata kazi aliyotaka. Anasema: “Nilijifunza kukubali kazi yoyote inayofaa. Kwa kipindi fulani nilifanya kazi ya kuuza vitu dukani. Pia niliuza chapati barabarani na kusafisha nyumba. Mwishowe, nilipata kazi ambayo nilikuwa nimesomea.”

Mary, mmoja wa rafiki zangu wa karibu sana, aliwahi kuachana na kazi yake ya ukarani, aliona umuhimu wa kubadilikana. Anaeleza: “Sikusisitiza kwamba lazima nipate kazi ileile ambayo nilikuwa nikifanya. Nilichunguza kila kazi niliyotajiwa, hata kama ilikuwa kazi ambayo watu huiona kuwa ya hali ya chini. Kwa sababu hiyo, nilifaulu kupata kazi iliyoniwezesha kuwategemeza watoto wangu wawili.”

4. Toa Habari Kamili Kuhusu Elimu na Ujuzi (CV)
Wale wanaotoa maombi ya kazi za usimamizi, lazima waandike na kusambaza habari kuhusu elimu na ujuzi wao. Lakini hata iwe unatafuta kazi gani, habari kamili kuhusu elimu na ujuzi ulio nao inaweza kusaidia sana. Nigel, mshauri wa kazi kwa muda mrefu, anasema: “Habari kuhusu elimu na ujuzi wako huwafahamisha waajiri juu yako na mambo ambayo umetimiza na kwa nini wanakuhitaji.”

Utaandika habari gani? Andika jina lako kamili, anwani, namba ya simu, na anwani ya barua-pepe. Taja lengo lako. Taja elimu uliyo nayo na pia mazoezi na stadi ambazo umepata zinazohusiana na kazi unayotafuta. Toa habari kamili kuhusu kazi ambazo umefanya hapo awali. Taja ulichofanya na pia miradi uliyofikia na manufaa uliyoletea kampuni uliyokuwa ukifanyia kazi. Pia taja mambo uliyofanya katika kazi yako ya awali ambayo yanafanya ustahili kazi unayotafuta. Tia ndani habari za kibinafsi zinazofafanua sifa na mapendezi yako. Kwa kuwa mahitaji ya kampuni hutofautiana, huenda ukahitaji kubadili habari unazotoa kila unapotoa maombi ya kazi.

Je, unapaswa kutoa habari kuhusu elimu na ujuzi wako ikiwa unatafuta kazi kwa mara ya kwanza? Ndiyo! Huenda umefanya mambo mengi yanayoweza kuonwa kuwa ujuzi wa kazi. Kwa mfano, je, unapenda useremala au labda kurekebisha magari makuukuu? Unaweza kutaja mambo hayo. Je, umewahi kufanya kazi yoyote ya kujitolea? Taja kazi ya kujitolea ambayo umewahi kufanya na miradi uliyofikia.

Usipopata nafasi ya kumwona mtu unayetazamia akuajiri, acha kadi ndogo, ikiwezekana yenye ukubwa wa sentimeta 10 kwa sentimeta 15 (business card), ambayo ina jina, anwani, namba ya simu, na anwani ya barua-pepe, kutia ndani maelezo mafupi kuhusu ustadi wako na mambo ambayo umetimiza. Ikifaa, unaweza kubandika picha yako nyuma ya kadi hiyo. Wape kadi hiyo watu ambao wanaweza kukusaidia kupata kazi na uwaombe wampe mtu yeyote wanayemjua ambaye ana kazi unayotafuta. Mwajiri akiona kadi hiyo, anaweza kukupa nafasi ya mahojiano, au labda akuajiri!

Kuandika habari kuhusu elimu na ujuzi wako kunaweza kufanya uhisi ukiwa na uhakika unapotafuta kazi. Wataalam wa masuala ya kazi wanashauri ifuatavyo: “Kuandika habari kuhusu elimu na ujuzi wako kunaweza kukusaidia upange mawazo na miradi yako. Pia kunafanya uwe na uhakika kwa sababu kutakusaidia ujitayarishe kwa ajili ya maswali ambayo huenda ukaulizwa wakati wa mahojiano ya kazi.”

Leo hii teknolojia imerahisisha mambo. Waweza kufanya hayo yote kupitia mtandao wa kijamii wa watu wenye taaluma ujulikanao kama LinkedIn. Mtandao huu ni maalum kwa ajili ya kukuunganisha wewe na mwajiri.

5. Jitayarishie Mahojiano Vizuri
Utajitayarishaje kwa ajili ya mahojiano? Huenda ukataka kufanya utafiti kuhusu kampuni unayotaka kufanyia kazi. Kadiri unavyojua mengi kuhusu kampuni hiyo, ndivyo utakavyojieleza vizuri wakati wa mahojiano. Pia utafiti wako utakusaidia kujua ikiwa kweli kampuni hiyo ina kazi unayotaka au kama ungependa kuifanyia kazi.

Kisha, fikiria mavazi utakayovaa unapoenda kwenye mahojiano. Ikiwa kazi unayotafuta inahusisha kazi ngumu, valia mavazi safi, nadhifu, na yanayofaa kazi hiyo. Kuvalia na kujipamba kwa njia nadhifu kutamwonyesha mtu unayetazamia akuajiri kwamba unajiheshimu na hivyo yaelekea utajivunia kazi yako. Ikiwa unatazamia kufanya kazi ya ofisi, vaa mavazi ambayo huonwa kuwa yanafaa kazi hiyo mahali unapoishi. Edwini yeye anashauri: “Chagua mavazi yako muda mrefu kabla ya wakati unapopaswa kwenda kwenye mahojiano ya kazi ili usifanye mambo harakaharaka na kuwa na mkazo mwingi kabla ya mahojiano.”

Pia ninapendekeza ufike dakika 15 hivi kabla ya mahojiano. Bila shaka, si jambo la hekima kufika mapema sana. Lakini pia kufika ukiwa umechelewa kunaweza kuharibu mambo. Wataalamu wanasema kwamba sekunde tatu za kwanza za mahojiano ni muhimu sana. Katika sekunde hizo, yule anayekuhoji hukagua sura yako na tabia yako, mambo ambayo huamua maoni yake kukuhusu. Ukichelewa, atakuwa na maoni mabaya kukuhusu. Kumbuka kwamba hutapata nafasi nyingine ya kurekebisha maoni ambayo mtu hupata kukuhusu mara ya kwanza.
Pia, kumbuka kwamba yule anayekuhoji si adui yako. Huenda yeye pia alitoa ombi kwa ajili ya kazi yake, kwa hiyo anajua jinsi unavyohisi. Kwa kweli, huenda akawa na wasiwasi kwa kuwa labda hajazoezwa vya kutosha kuwahoji watu. Isitoshe, ikiwa yule anayekuhoji ndiye mwajiri, huenda akapata hasara kubwa akiajiri mtu asiyefaa.

Ili uanze vizuri, tabasamu na umsalimu yule anayekuhoji kwa mkono ikiwa hiyo ni desturi ya kwenu. Wakati wa mahojiano, fikiria hasa mambo ambayo mwajiri anatarajia kutoka kwako na yale unayoweza kutimiza. Wakati wa mahojiano, jitahidi kuyaepuka haya: Usisimame, kuketi au kutembea kizembe. Utulivu huonyesha kwamba mtu ana uhakika. Usizungumze sana au kwa urafiki sana, wala usitumie lugha chafu kamwe. Pia epuka kuwachambua waajiri na wafanyakazi wenzako wa awali kwa kuwa ukifanya hivyo yule anayekuhoji ataona kwamba utachambua kazi hiyo pia.

Wataalamu wanapendekeza ufanye na kusema mambo yafuatayo wakati wa mahojiano: Mtazame yule anayekuhoji, tumia ishara za kawaida unapozungumza, na uzungumze kwa ufasaha. Jibu maswali kifupi na kwa unyoofu, na uulize maswali yanayofaa kuhusu kampuni hiyo na kazi unayotarajia kufanya. Omba kazi hiyo baada ya mahojiano ikiwa bado unaitaka. Kufanya hivyo kutaonyesha kwamba bado unataka kazi hiyo.
Ukifuata mapendekezo yaliyoonyeshwa juu, huenda ukapata kazi karibuni. Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini ili uidumishe?

NYONGEZA: Jihadhari sana na kuandika mambo yasiyofaa kwenye kurasa zako katika mitandao ya kijamii. Hii ni kwa sababu wa-ajiri wengi huwa wanayachunguza mawazo yako kwa kuzitembelea kurasa zako katika mitandao ya kijamii kabla na baada ya kukuita kwenye mahojiano.

Lakini pia kama umemaliza chuo na ungependa kujiajiri mwenyewe katika biashara pamoja na kuwasidia vijana wengine, hakikisha tunawasiliana haraka iwezekanavyo. Wanahitajika vijana wasiozidi 3 watakaotusaidiakatika mradi wetu wa sasa wa kukuzakiwango cha ajira hapa nchini. Kama uko Dar es Salaam na ungependa miongoni mwa hao vijana watatu, wahi mapema. Nipigie +255 684524265.


No comments:

Post a Comment