Mkuu wa Jeshi hilo IGP, Ernest Mangu.
Uchunguzi wa kina ambao umefanywa na TONYTZ.BLOG kwa takribani wiki
tatu sasa umebaini kuwa hatua ya baadhi ya askari polisi kuasi ndani ya
jeshi hilo kunatokana na kuchukizwa na mambo kadhaa yaliyofanywa na IGP
Mangu tangu alipoteuliwa na Rais Jakaya Kikwete kushika wadhifa huo.
Baadhi ya watumishi wa serikali waliozungumza na gazeti hili kwa
nyakati tofauti walisema mambo ambayo yamechukizwa baadhi ya watu ndani
ya jeshi hilo ni kutokana na kufukuzwa kazi askari wengi na wengine
kubadilishwa vituo vyao vya kazi kwa sababu mbalimbali, mambo ambayo
yamefanyika kipindi cha IGP Mangu.
“Unakumbuka wakati Sanya (Laurance Sanya) alipokuwa RPC Mbeya
kulitokea tukio moja la uvamizi wa Kituo cha Polisi Tunduma lakini
kipindi cha utawala wa IGP Mangu yamejitokeza mengi hapa kuna sababu,”
alisema.
Alisema IGP Mangu amekuwa mkuu wa Jeshi la Polisi ambaye ameongoza
kufukuza askari hususani wanaokula rushwa ambao hakuwavumilia na ndiyo
hao hao wamegeuka kuwa adui wa jeshi hilo kwa kushirikiana na jamaa na
ndugu zao ambao bado wapo ndani ya utumishi wa jeshi hilo.
Jambo la pili lililojenga hasira kwa askari hao ni hatua ya IGP
Mangu kutoa tishio kwamba askari wote ambao wana vyeti vya kughushi
wajisalimishe.
“Taarifa za Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) inaonyesha
kuwa zaidi ya watumishi 10,000 wa Jeshi la Polisi wana vyeti vya
kughushi lakini kwa bahati mbaya katika awamu zote za utawala wahusika
wamekuwa wakiachwa bila kuchukuliwa hatua na sasa IGP Mangu amekuja
kuyavumbua,” kilisema chanzo kutoka ndani ya serikali.
Chanzo hicho kilieleza kuwa baada ya IGP Mangu kutoa tamko la
kutaka watumishi ndani ya jeshi hilo wenye vyeti vya kughushi
wajisalimishe ndipo matukio ya uvamizi wa vituo vya polisi yalipoibuka
kwa kasi ili mkuu huyo wa Jeshi la Polisi aonekane ameshindwa kazi na
kufukuzwa.
Anaeleza kuwa kuhusisha matukio ya uvamizi huo na suala la ugaidi
inaweza kuwa siyo kweli kwa asilimia kubwa kwa sababu mara nyingi
magaidi wanaofanya matukio makubwa mfano nchi jirani wanakuwa na silaha
kubwa kama AK-47 sasa inawezekanaje kama kweli ni magaidi hapa kwetu
wawe wanapora bunduki ndogo za SMG.
Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Hellen
Kijobisimba, alisema matukio ya uvamizi wa vituo vya polisi yameanza
kujitengeneza pole pole na sasa yamekuwa makubwa.
“Matuki ya vituo kuvamiwa yalianza kwa wananchi wenye hasira kutaka
kutoa watu waliokamtwa na baadaye wakaona kama kumbe ni rahisi kuvamia
kuiba silaha, kujeruhi askari na kuua,” alisema.
Alisema wakati hali ya kiuslama ikibadilika, Jeshi la Polisi kwa
upande wake bado halijabadilika ili kukabiliana na matukio hayo.
“Zamani usingeweza kuona askari anayetembea barabara ananyang’anywa
silaha hata kama huyo askari yukoje, lakini hivi sasa polisi wapo
kwenye doria wanavamia na kunyanng’anywa silaha, wanaenda kama vile
nyumbani kwao na bahati mbaya polisi wenyewe hawajashtuka,” alisema.
Kijobisimba alisema polisi wangekuwa wamebadilika kiutendaji matukio hayo yasingetokea.
Alisema sababu nyingine ya kuibuka kwa matukio hayo ni ndani ya
Jeshi la Polisi lenyewe kuna tatizo ambalo inabidi litafutiwe ufumbuzi.
“Ukiangalia tukio la uvamizi wa Kituo cha Polisi Stakishari ni
utata, mimi nilikuwa jeshini, utunzaji wa silaha unakuwa very secure
(usalama mkubwa), sasa wale Stakishari utunzani wao wa silaha unakuwaje
kiasi kwamba wavamizi waliingia mara moja na kuchukua silaha kama kweli
hakukuwa na inside job (kazi ya ndani),” alisema na kuongeza:
“Katika tukio hilo pengine inawezekana hata mfungaji wa mlango wa
kutunzia ofisi akawa alisahau kufunga kwani wavamizi wasingeweza kufika
kirahisi na kupora.”
Bikijobisimba alisema mambo hayo yanaweza sehemu ambayo kuna askari ambao siyo waadilifu kutokana na jinsi wanavyopewa mafunzo.
“Zamani kulikuwa na utaratibu mtu akitaka kuajiriwa polisi
wanaangalia urefu ndiyo wanachukuliwa, lakini leo hii hata wafupi wapo
wengine na inawezekana wanapelekwa na ndugu zao na pia mafunzo
yanatolewa kwa miezi sita wakati zamani ilikuwa miezi tisa,” alisema.
Alisema mafunzo ya miezi sita kimsingi hayawezi kutosha kumfundisha
askari kuwa katika maadili mazuri na mkakamavu kiasi cha kuaminiwa kuwa
mlinzi wa taifa.
Kijobisimba alisema ili kukabiliana na matukio hayo kuna umuhimu wa
Jeshi la Polisi kutafuta chimbuko la matukio ya uvamizi wa vituo vya
polisi kwani lazima kutakuwa kuna tatizo.
Naye mwanaharakati wa haki za binadamu, Julius Niselia, alisema
matukio hayo yanaonyesha kuwa mabadiliko ya uongozi ndani ya Jeshi la
Polisi yaliyomwingiza IGP Mangu hayakupokelewa vizuri ndani ya jeshi
hilo na baadhi ya askari waliokuwa watii kwa uongozi uliondoka ambao
wamekumbana na fagio la chuma la uongozi mpya na ndiyo wanaofanya njama
hizo.
“Mangu ni mkali sana hapendi askari wanaofanya uovu hivyo amekuwa
akichukua hatua haraka na kusababisha malalamiko kwa askari ambao
walilelewa vibaya ndani ya jeshi hilo na viongozi wapole wasiochukua
hatua,” alisema.
“Askari wanaofukuzwa kwa utovu wa nidhamu ndiyo wanaounda magenge
ya kihalifu ili kumdhoofisha IGP Mangu aonekani hafai kiutendaji,”
alisema.
Kwa upande wake, Askofu wa Kanisa la Pentekoste World Mission
International, Samson Mwalyego, alisema chanzo cha matukio hayo ni
kuporomoka kwa maadili ndani ya Jeshi la Polisi.
Alisema ndani ya jeshi hilo watumishi wanajali zaidi rushwa na
wamekuwa siyo wa siri wanapopewa taarifa jambo ambalo limewakatisha
tamaa wananchi kushirikiana nalo.
Wakati hayo yakiendelea baadhi ya askari polisi wamelalamikia
kitendo cha serikali kupuuza malalamiko yao mbalimbali ikiwamo ubaguzi
katika upandishaji wa madaraja na nyongeza ya kima cha mshahara tangu
miongoni mwao walipopandishwa vyeo Agosti, mwaka jana.
Taarifa za uhakika kutoka ndani ya jeshi hilo zinaeleza kwamba,
kutokana na hali hiyo kiwango cha utendaji kazi kwa polisi hao kimeshuka
kutokana na uongozi wa juu kukaa kimya.
Hata hivyo, imefahamika kwamba tatizo hilo limefanywa kuwa siri na hakuna askari anayeruhusiwa kuzungumzia kwa uwazi.
Askari wachache ambao walikuwa mstari wa mbele kufuatilia suala
hilo, imedaiwa sasa wamenyamazishwa baada ya kupewa stahiki zao
kinyemela.
“Tumevumilia vya kutosha jambo hili, hivi vyeo tulivyopewa ni kama
hewa, tukiuliza ngazi za juu hawatupatii majibu ya kuturidhisha,”
kilisema chanzo kimoja.
Mmoja wa askari hao ambaye alitaka jina lake lisitajwe, alisema
malalamiko hayo yanawahusu askari wengi nchi nzima ambao walikwenda
katika mafunzo mwaka jana.
Alisema licha ya kufanya vizuri na kupandishwa vyeo mbalimbali vya
kijeshi, mishahara yao imebaki kama mwanzo jambo ambalo limewarudisha
nyuma kiutendaji.
“Huwezi kufanya kazi nzuri katika hali hii, tunachoomba serikali isikilize kilio chetu na kututatulia,” alisema askari huyo.
Askari mwingine alisema huko nyuma waliunda kamati maalum ya
kufuatilia suala hilo ngazi za juu za jeshi hilo, lakini walikatishwa
tamaa baada ya kuona kuna tatizo katika mchakato wa kuwaongezea maslahi.
“Jambo la kusikitisha watu wachache walionekana wasemaji
waliingiziwa pesa za nyongeza, tuliobaki hatujui tutafikiwa lini na
hakuna anayethubutu kusema kwa uwazi ili kulinda kibarua chake,”
alisema.
TUME YAUNDWA
Askari hao walidai mwanzo wa mwaka huu serikali ilifanya uhakiki wa
watu wanaotakiwa kuongezewa mishahara kulingana na nafasi zao za kazi.
Alisema licha ya kupewa ushirikiano na askari hao katika vituo
vyote walivyotembelea, hadi sasa hakuna jibu lolote walilopewa, badala
yake walitakiwa kuukaa kimya.
“Tunajua IGP anajua tatizo hili vizuri, tunamuomba atusikilize malalamiko yetu na kuyafanyia kazi kwa haraka,” alisema.
VITUO VILIVYOVAMIWA
Katika kipindi cha kuanzia Juni, 2014 mpaka Julai 13, mwaka huu,
bunduki 53 zimeporwa katika matukio ya uvamizi wa vituo vya polisi na
askari 11 kuuawa.
Vituo vya polisi vilivyovamiwa ni Newala mkoani Mtwara, ambako
bunduki tatu ziliporwa, mkoani Pwani katika wilaya ya Ikwiriri (bunduki
saba), Kimanzichana, wilaya ya Mkuranga (bunduki tano) mbili zikiwa za
polisi na tatu za raia zilizokuwa zimezihifadhiwa.
Vingine ni Kituo cha Polisi Ushirombo wilaya ya Bukombe, mkoani
Shinyanga bunduki 18 ziliporwa, ingawa baadaye zilipatikana zote.
Kituo cha Polisi Pugu Machinjioni, mkoani Dar es Salaam na Tanga,
askari waliokuwa katika shughuli za ulinzi na doria walishambuliwa na
kuporwa silaha tatu na Kituo cha Polisi Stakishari, Dar es Salaam ambako
bunduki 20 ziliporwa na askari wanne na raia watatu kuuawa.
No comments:
Post a Comment