Madhara ya kimbunga Haiyan Ufilipino
Meli za Marekani na Uingereza
zinaelekea nchini Ufilipino huku Umoja wa Mataifa ukiomba msaada
kupelekwa nchini humo kukiwa na taarifa za uharibifu mkubwa
uliosababishwa na kimbunga Haiyan.
Marekani imepeleka ndege na meli za mizigo kwenda Ufilipino, wakati ambapo Uingereza imepeleka meli ya kivita.
Watu wapatao 10,000 wanahofiwa kufa, na maelfu ya walionusurika katika kimbunga Haiyan wanahitaji msaada.
Rais wa Ufilipino Benigno Aquino ametangaza hali hiyo kuwa janga la kitaifa.
Katika taarifa yake, Rais Aquino,amesema majimbo
mawili ya Leyte na Samar yameathirika zaidi kutokana na kimbunga hicho,
ikiwemo watu wengi kupoteza maisha.
Juhudi kubwa za kimataifa zinafanyika ili kutoa
msaada wa dharura kwa Ufilipino, lakini wafanyakazi wa mashirika ya
kutoa msaada wanakwama kuyafikia maeneo yaliyokumbwa na kimbunga.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon
amezielezea picha zinazoonyesha ya kimbunga hicho kuwa zinatisha na
kukatisha tamaa.
Umoja wa Mataifa utazindua mpango mkubwa wa
msaada wa kibinadamu, na kutenga dola milioni 25 kusaidia jitihada za
misaada ya dharura.
"Maelfu ya watu wameripotiwa kufa na watu
wapatao milioni kumi wameathirika kutokana na kimbunga hicho. Hebu
tuonyeshe mshikamano wetu na watu wa Ufilipino katika kipindi hiki cha
kuhitaji msaada," amesema.
Mbali na Marekani na Uingereza, nchi nyingine
pia zimeahidi mamilioni ya dola ukiwa ni msaada kwa Ufilipino. Australia
imeidhinisha dola milioni 9, wakati ambapo New Zealand imeahidi zaidi
ya dola milioni moja, huku Uchina ikiahidi kutoa dola laki
moja.($100,000)
No comments:
Post a Comment