Wanaume ni dhaifu kuliko wanawake! Nani anabisha?
Ninaamini hivyo kwa sababu kuna mambo kadhaa ambayo yamenipa ushahidi
kwamba, mwanaume hata akijidai kwamba ana ubavu wa kiwango gani, lakini
bado kiufahamu ni mtumwa wa mwanamke. Kuna mambo makuu kama matatu
ambayo yananifanya nifikiri hivyo.
Kwanza ni ile hali ya mwanaume kuweza kutawaliwa na mwanamke wa nje (aka
nyumba ndogo) na kukubali kuacha familia yake na hata kuvunja heshima
yake. Kuna wakati najiuliza kama kweli mwanaume mbele ya mwanamke huwa
anaweza kutumia akili yoyote. Unakuta mwanaume anakutana na mwanamke
barabarani na kumtongoza na akikubaliwa anamgeuza huyo mwanamke kuwa
nyumba ndogo yake, lakini usidhani kwamba nyumbani kwa huyo mwanaume
kuna matatizo ya ndoa. Hapana, hakuna tatizo lolote ila mwanaume huyo
kaendeshwa na tamaa yake ya mwili na akashindwa kuidhibiti. Matokeo
yake anajikuta analowea huko kwa nyumba ndogo yake, hadi anaharibikiwa.
Hajali watoto, hajali mkewe, hajali heshima yake wala chochote.
Unakuta mwanaume anazuzuliwa na shanga tu, au kitu kingine kidogo sana,
labda weupe wa mkorogo au lipstiki na makalio makubwa. Kwa ujumla utaona
kabisa kwamba, ufahamu wa mwanaume ni kama ziro kabisa. Halafu kumbuka
kwamba, wakati huo hiyo nyumba ndogo inajuwa kabisa kwamba, inalisanifu
hilo janamume b.w.e.g.e, au tuite buzi lakini limo tu, kama GEGEREKA.
Kama mwanaume angekuwa na ufahamu kuliko mwanamke, angeweza vipi
kushikwa na nyumba ndogo kwa kiwango cha kukatisha tamaa kwa kiasi
hicho? Ni wazi mwanamke ndiye ambaye ana uwezo mkubwa zaidi wa kufikiri
na kupanga. Kama mwanaume angekuwa na ufahamu wa kutosha, si angeweza
basi kung’amua kwamba, anasanifiwa na nyumba ndogo, kwani hapo hakuna
kupendwa bali kuchunwa.
Pili ni ile hali ya mwanaume kupenda kutatua mambo yake kwa mabavu
badala ya kufikiri. Ukiangalia sana, kwenye matatizo au vurugu nyingi,
wanawake huwa ni watu wa hekima zaidi kuliko ubabe, yaani wanatumia
vichwa vyao kuliko miili. Siyo kwamba, wanaogopa kutumia miili yao,
hapana. Kuna mazingira ambayo unaona kabisa kama mwanamke angeamua
kujikaza hapa, hakika angempiga huyu mwanaume. Lakini sisi wanawake
tunapenda kuyamaliza mambo kwa hekima na uelewano.
Hii ni hekima ambayo kwa bahati mbaya kwa wanaume wengi sana
haipatikani. Kwa hiyo, unaona kabisa kwamba, mwanaume bado yuko kwenye
ile hali au kiwango cha chini cha kujifahamu kwa sababu bado yuko kwenye
kuamini mabavu yake.
Tatu, mwanamke ni bora zaidi kuliko mwanaume katika suala la kukabiliana
na matatizo na vurugu za kimaisha. Unaweza kuona mwanamke ametelekezwa
na mume akiwa na watoto, lakini hata siku moja hachukui uamuzi wa
kuwakimbia watoto. Ni wanawake wachache sana kwa idadi ambayo hatuwezi
kuizingatia, ambao wanaweza kufanya hivyo.
Lakini kila siku magazetini kuna taarifa za ukatili wa wanaume dhidi ya
wanawake au wanaume kutelekeza familia zao. Ukiangalia sana utaona
wamekimbia familia zao kwa sababu ya nyumba ndogo au kwa sababu ya ugumu
wa maisha. Kwa nini msione kwamba, mwanamke bado ni shujaa zaidi ya
mwanaume…?
No comments:
Post a Comment